Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Saturday, December 24, 2016

SIMBA KILELENI HADI MWAKA 2017






USHINDI wa bao 1-0 iliyoupata Simba leo katika Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya JKT Ruvu umeiwezesha kuongeza pengo la pointi dhidi ya Yanga timu inayoshika nafasi ya pili.
Simba kwa ushindi huo imefikisha pointi 41 ikiendelea kuongoza msimamo wa ligi hiyo ikifuatiwa na Yanga yenye pointi 37.
Kabla ya mechi za raundi ya 17 kuchezwa jana na leo, Simba na Yanga zilikuwa zinatofautiana pointi mbili, lakini mambo yalianza kubadilika jana baada ya Yanga kutoka sare ya bao 1-1 na African Lyon na kisha Simba leo kuibuka na ushindi huo.
Ni wazi kuwa pengo hilo la pointi litaongeza ushindani zaidi katika ligi hiyo, ambapo Jumatano Yanga itacheza na Ndanda FC Uwanja wa Uhuru kisha siku inayofuata Simba itacheza na Ruvu Shooting uwanja huohuo.
Katika mchezo huo wa jana, bao hilo pekee lilifungwa dakika ya 45 na Muzamir Yassin akiunganisha krosi ya Javier Bukungu.
Hata hivyo bao hilo lilizua malalamiko kwa wachezaji wa JKT Ruvu, wakidai kipa wao, Hamis Seif aliumia katika harakati za kuokoa mpira na alianguka chini, hivyo mwamuzi Hans Mabena wa Tanga alipaswa kupuliza filimbi kwa kuwa wachezaji wa Simba hawakutoa mpira nje kwa kufuata taratibu za Fair Play.
Lakini badala yake wakati kipa huyo akiwa chini, Simba waliendelea kucheza na kufunga bao hilo.
Hata hivyo hatua ya kipa huyo kuanguka wakati Simba wakishambulia lango lake haikuwashtua wengi kwa vile katika kipindi hicho cha kwanza alianguka zaidi ya mara tatu akitibiwa na kuendelea na mchezo, hivyo hata tukio hilo ilionekana kama ni utaratibu wake uleule.
Kipindi cha kwanza JKT Ruvu walijaribu kufika langoni kwa Simba mara kadhaa, lakini walikosa mbinu za kuipenya ngome ya Simba, huku wenzao wakifika mara nyingi langoni lakini umaliziaji ulikuwa hafifu.
Wachezaji wa Simba wakiongozwa na Shiza Kichuya, Muzamir na Pastory Athanas nao watajilaumu kutokana na kushindwa kutumia nafasi walizopata kwa nyakati tofauti kufunga.
Kipindi cha pili Simba iliendelea kupoteza nafasi nyingi za kufunga, huku JKT Ruvu inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) ikifanya mashambulizi ya kushtukiza, lakini umaliziaji ulikuwa butu. JKT Ruvu ina pointi 13 na inashika nafasi ya 15.
Nayo timu ya Majimaji ya huko na Azam FC zimefungana bao 1-1 katika mfululizo wa ligi hiyo.
Kutokana na matokeo hayo Azam imefikisha pointi 27 ikiendelea kushika nafasi ya tatu nyuma ya Yanga, huku Majimaji ikifikisha pointi 17 ikiwa nafasi ya 14 kati ya timu 16 zinazoshiriki ligi hiyo.
Azam ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 17 mfungaji akiwa Yahya Mohammed kabla ya Majimaji kusawazisha dakika ya 67 mfungaji akiwa Alex Kondo.
Matokeo mengine, Mtibwa iliifunga Ndanda FC mabao 2-0 Uwanja wa Nang’wanda Sijaona, Mtwara. Mbeya City na Toto Africans zilitoka 0-0, huku Kagera Sugar ikiifunga Stand United bao 1-0 na Mwadui ikiifunga Mbao FC bao 1-0.

No comments:

Post a Comment