BAO la kusawazisha la Azam lililofungwa na John Bocco leo, limefanya Yanga na Azam kumaliza msimu wa Ligi Kuu Tanzania Bara kukiwa
hakuna mbabe kati yao baada ya kufungana mabao 2-2 Uwanja wa Taifa, Dar es
Salaam.
Mchezo wa kwanza baina ya timu hizo katika ligi hiyo
Oktoba mwaka jana katika uwanja huohuo, zilitoka sare ya bao 1-1 na jana
ulikuwa wa marudiano katika raundi ya 21 ya ligi hiyo, huku zenyewe ikiwa ni
raundi ya 20.
Mechi
15 zilizopita baina ya timu hizo katika ligi zimeshindwa kumtoa ‘mbabe,’ kila
timu imefanikiwa kushinda mara 5 na michezo mingine mitano ikimalizika kwa
matokeo ya sare.
Timu
hizo zilikutana katika robo fainali ya michuano ya Kombe la Kagame Julai mwaka
jana, ambapo hadi muda wa kawaida unamalizika matokeo yalikuwa 0-0, Yanga
wakapoteza kwa changamoto ya mikwaju ya penalti na kuondolewa katika michuano
ambayo Azam FC walitwaa ubingwa.
Zikakutana
tena katika mchezo wa Ngao ya Jamii Septemba, 2015 na kwa mara nyingine tena
dakika 90 zilimalizika kwa matokeo ya 0-0, safari hii Yanga walishinda katika
mikwaju ya penalti.
Baada
ya sare ya 1-1 katika mechi ya Ligi Kuu Desemba mwaka jana, timu hizo
zilikutana tena Januari mwaka huu katika hatua ya makundi ya michuano ya Kombe
la Mapinduzi Zanzibar na zilifungana bao 1-1.
Kutokana na matokeo ya jana, Yanga inaendelea kuongoza
ligi hiyo ikiwa na pointi 47 sawa na Azam, lakini Yanga ina uwiano mzuri wa
mabao ya kufunga na kufungwa.
Simba yenyewe inashika
nafasi ya tatu ikiwa na pointi 45 ikicheza michezo 20 sawa na Yanga, ambapo leo
Simba itashuka kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kucheza na Mbeya City.
Kama Simba itashinda mchezo
wa leo itafikisha pointi 48 na kushika usukani wa ligi, ingawa itakuwa mbele
mchezo mmoja ukilinganisha na Azam na Yanga.
Katika mchezo wa jana, Azam
ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 11 baada ya beki Juma Abdul kujifunga
katika harakati za kuokoa.
Bao hilo lilionekana
kumchanganga beki huyo na dakika ya 28 Juma Abdul alisahihisha makosa yake kwa
kuifungia Yanga bao la kusawazisha kwa shuti kali nje ya eneo la 18 kutokana na
pasi ya Donald Ngoma.
Yanga iliendelea kulisakama
lango la wapinzani wao na dakika ya 41 ilipata bao la pili mfungaji akiwa Ngoma, kutokana na krosi ya Amis Tambwe.
Washambuliaji wa timu zote
waliendelea kufika katika maeneo ya hatari, lakini tatizo la umaliziaji
lilikuwa likiwaathiri.
Dakika ya 70, John Bocco
alifunga bao la kusawazisha baada ya kupokea pasi ya Kipre Tchetche, bao ambalo
liliwanyanyua vitini mashabiki wa Simba timu yenye utani wa jadi na Yanga na
kuanza kushangilia.
Mashabiki hao wa Simba
walikuwa wakishangilia wakiamini ni fursa nzuri kwa timu yao kukaa kileleni
kama itaifunga Mbeya City.
Hata hivyo, mchezo wa Mbeya
City utakuwa na ushindani mkubwa kutokana na mazingira ya timu zote mbili
katika msimamo huku Mbeya City ikiwa nafasi ya 10 katika msimamo kutokana na
pointi zake 21.
Yanga: Ally Mustafa
‘Barthez’, Juma Abdul, Mwinyi Hajji Mngwali, Kevin Yondan, Vincent Bossou,
Mbuyu Twite, Simon Msuva/Godfrey Mwashiuya, Thabani Kamusoko, Amissi
Tambwe/Pato Ngonyani, Donald Ngoma na Deus Kaseke.
Azam FC; Aishi Manula,
Shomary Kapombe, David Mwantika, Said Mourad, Serge Wawa, Farid Mussa/Didier
Kavumbangu, Jean Baptiste Mugiraneza, Himid Mao/Frank Domayo, Ramadhani Singano
‘Messi’/Mudathir Yahya, John Bocco na Kipre Tchetche
Naye Alexander Sanga
anaripoti kutoka Mwanza kuwa timu ya Toto Africans na Ndanda FC ya Mtwara jana
zilitoka 0-0 katika Uwanja wa CCM Kirumba.
Wachezaji wa Ndanda FC
walimlalamikia mwamuzi Abdallah Kambuzi wa Shinyanga wakidai alilikataa bao la
Atupele Green dakika ya 89 wakati lilikuwa halali.
No comments:
Post a Comment