Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Friday, August 9, 2013

RODGERS AMPA ADHABU SUAREZ KWA KUTAKA KUTUA ARSENAL

Liverpool, England 
MSHAMBULIAJI wa Liverpool, Luis Suarez, amenyanyapaliwa na Kocha wa timu hiyo, Brendan Rodgers, kwa kutoruhusiwa kufanya mazoezi na wenzake, kwa madai ya kutoiheshimu klabu, jambo ambalo sasa limemfanya kujifua na mwanawe.

Juzi ilidaiwa kuwa Suarez ndiye aliyekataa kujifua na wenzake, lakini jana siri hiyo ilifichuka, huku Rodgers pia akipinga kauli ya nyota huyo wa Kimataifa wa Uruguay kuwa aliahidiwa kuruhusiwa kuhama majira haya ya joto endapo Liverpool haitafuzu Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Suarez, 26, pia amekerwa na kitendo hicho na sasa wiki hii amepanga kuwasilisha ombi lake la kutaka kuondoka Anfield, endapo ataendelea kuzuiwa kuhama, na kama haitoshi ataishitaki kwa Chama cha Soka England, FA.

"Hakuna aina hiyo ya ahadi iliyofanywa, wala ahadi iliyovunjwa," alisisitiza Rodgers, akimzungumzia Suarez, ambaye msimu uliopita alifunga mabao 30 katika mechi 44 alizoichezea Liverpool.

Tangu ajiunge na timu hiyo akitokea Ajax Januari 2011 kwa ada ya pauni milioni 22.7 (Sh. bilioni 55 za Tanzania), ameifungia Liverpool mabao 51 katika mechi 96 alizoichezea. Akiwa Ajax alifunga mabao 49 katika mechi 48, huku Uruguay akiifungia mabao 35 kwenye mechi 69.

"Liverpool imekuwa na mazungumzo ya mara kwa mara na wawakilishi wa Suarez na inajua wazi mtazamo wake. Kwa ujumla kumekuwa na ukosefu wa nidhamu kwa klabu ambayo imempa kila kitu."

Chanzo kimoja kilichopo karibu na miamba hiyo ya Anfield, kilisisitiza kuwa uamuzi wa Suarez kutakiwa kufanya mazoezi peke yake ulitolewa kabla hata hajaanza 'kubwatuka', ambapo alifanya hivyo Jumanne.

Rodgers aliongeza: "Nitaendelea kuchukua maamuzi magumu. Nadhani Luis anatambua ni kwa jinsi gani anapata sapoti kutoka klabuni, kitu ambacho amekuwa akikipata kwa msimu mzima uliopita.

"Kazi yangu ni kupigana katika kuilinda klabu. Mazungumzo ninayoyafanya kuhusu yeye ninayo na yataendelea kubaki kuwa siri."

Arsenal imeshatoa ofa mbili ambazo zimekataliwa na Liverpool, ya mwisho kati ya hiyo ilikuwa ni pauni milioni 40 (Sh. bilioni 97.2 za Tanzania) na pauni moja zaidi ambayo itaiwezesha kufikia kigezo cha kuweza kuvunja mkataba wa Suarez.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa Chama cha Wachezaji wa Kulipwa, Gordon Taylor alifafanua kuwa hakuna kipengele katika mkataba wa mchezaji ambacho kinaeleza kuwa Liverpool italazimika kumuuza endapo itapewa ofa zaidi ya pauni milioni 40.

"Kama kutakuwa na ofa chini ya pauni milioni 40, pande mbili zitaketi na kuijadili, lakini hauelezi kuwa klabu itamuuza," alisema Taylor.



No comments:

Post a Comment