Dkt. Kikwete: Tumeridhishwa na Utekelezaji wa Miradi ya Afya ya JMKF Tabora
Rais
Mstaafu, Muasisi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi ya Jakaya Mrisho
Kikwete Foundation (JMKF), Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ameeleza kuridhishwa
kwake na kukamilika kwa ujenzi wa zahanati na utekelezaji wa Mradi wa Jamii
Salama mkoani Tabora.
Akizungumza
baada ya ziara yake ya siku nne ya kukagua miradi hiyo katika vijiji vya
Gengesita (Wilaya ya Uyui) na Ipembe (Wilaya ya Sikonge), Dkt. Kikwete
alibainisha kuwa zahanati hizo zimeshaanza kutoa huduma kwa wananchi.
Aidha aliishukuru
Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa
ushirikiano wake na JMKF, pamoja na kuishukuru kampuni ya Marekani ya S.C.
Johnson & Son kwa kufadhili miradi hiyo iliyolenga kusogeza huduma za afya
karibu na wananchi wa maeneo ya pembezoni.
Zahanati
hizo zimejengwa kutoa huduma kamili za afya ya msingi, ikiwemo idara ya
wagonjwa wa nje, kliniki ya afya ya uzazi na mtoto, wodi ya wazazi, vyoo vya
umma, kichomea taka, mashimo ya kondo la nyuma, na nyumba mbili za watumishi
ili kusaidia upatikanaji na uwepo wa kudumu wa wataalamu wa afya, hasa wauguzi
wakunga, maeneo hayo ya mbali.
Utekelezaji
wa miradi hii unatoa suluhu ya kudumu kwa changamoto ya muda mrefu ya umbali
mkubwa uliokuwa ukiwakabili wakazi wa vijiji hivyo—vikiwa takribani kilomita
152 kutoka makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uyui na kilomita 199 kutoka
Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge—hali iliyokuwaikosesha wajawazito, watoto,
wazee na wagonjwa huduma za haraka.
Hatua
hii ya ujenzi inatokana na mafanikio ya kliniki tembezi zilizoendeshwa na JMKF
mwanzoni mwa mwaka 2025 ambapo mamia ya kina mama wajawazito walipatiwa huduma
bila malipo. Kutokana na ukubwa wa mahitaji yaliyoshuhudiwa, JMKF iliamua
kujenga zahanati hizo ili kuweka msingi wa huduma za kudumu.
Kupitia
mafanikio hayo, JMKF imesema itaendelea kushirikiana na Serikali, wadau wa
maendeleo na sekta binafsi katika kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya
kwa jamii zinazoishi katika maeneo yenye changamoto ya kufikia vituo vya
kutolea huduma.



.jpeg)







Post a Comment