Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Monday, May 29, 2017

Mourinho kawapa Man U utukufu lakini …



Gullit: Wayne Rooney situation proves Jose Mourinho is Sir Alex Ferguson's true successor

NJIA aliyopitia imemfikisha katika ‘utukufu’ aliotaka kuwafikisha Manchester United, lakini bado Jose Mourinho ana mengi ya kujifunza na kufanyia kazi.
Alionesha mkato wa tamaa kwenye Ligi Kuu ya England (EPL) ngwe ya mwisho kiasi kwamba alifika mahali na kusema hawakuwa wakitaka kucheza mechi hizo tena, bali kujielekeza kwenye ligi ndogo – Europa League.
Alishaona kwamba hawana ubavu wa kuwapiku Arsenal, Liverpool wala Manchester City katika kuwania nafasi ya tatu na ya nne ili kufuzu kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya (UCL), ambayo ni ndoto kubwa ya klabu na wachezaji wengi hapa Ulaya.
Ni kwa sababu hiyo, bila wengi kujua awali, Mourinho alijiongoza kwenye Ligi ya Europa, akafanikiwa kupenya robo, nusu na hatimaye fainali, akakunja kidole na kusema hapo hapo, huku akimwaga makinda kwenye mechi za EPL.
Kweli amefanikiwa kuwapa ubingwa wa Europa Manchester United – kwa kuwafunga Ajax 2-0 – walau akamalizia msimu wake wa kwanza hapo kwa kutwaa kombe, tofauti na klabu hasimu – Manchester City wanaofundishwa na Pep Guardiola aliyekuwa pia kwenye msimu wake wa kwanza.
Sasa Man U wameungana na mabingwa wa England, Chelsea ambao chini ya Antonio Conte, naye kwenye msimu wake wa kwanza wametwaa kombe hilo wakati Tottenham Hotspur wamekuwa wakali zaidi chini ya Mauricio Pochettino na kushika nafasi ya pili, akijijengea matumaini ya kuwa kwenye ushindani mkubwa zaidi mwakani na akifikiria pia kutwaa ubingwa.
Wakati wachezaji wa Man U wakishangilia kutwaa kombe hilo Jumatano, Mourinho alikuwa akitembea akiwa na bendera nyekundu, akapitiliza mbele ya kikosi chake na kujaribu kwenda kupandikiza kamlingoti ka bendera hiyo uwanjani lakini kutokana na ugumu wa dimba mlingoti ukapinda.
Alijaribu zaidi lakini akashindwa, ikawa kama alivyojaribu kupata kufuzu kupitia EPL akashindwa akajielekeza ligi hiyo ndogo; hapo alisogelea kibango kilichokuwa hapo kikiwa kimeandikwa ‘Stockholm Final 2017’.  Hili lilikuwa hakika fumbo baada ya kashikashi zote kwenye ligi, kukaa nafasi ya saba muda mwingi, wakapanda ya sita kisha ya tano, wakapata majeruhi kabla ya kurudi chini nafasi ya sita walikomalizia.
Haikuishia hapo, Paul Pogba akafiwa na baba yake na kukosa mechi kadhaa, huku Zlatan Ibrahimovic aliyekuwa na uchu wa kuwa kwenye nne bora akiumia vibaya goti na hadi fainali hiyo inafanyika alikuwa akitembelea magongo, basi Man U wakawa wazito na wakagongwa na Arsenal waliokatisha muda wao mrefu wa kutofungwa mechi EPL.
Baada ya madhila yote hayo, hatimaye wamemaliza msimu kwa kikombe hicho kidogo, lakini maana yake kubwa ni kule kufuzu kwa UCL, ambapo msimu ujao watakuwa wakiwacheka wapinzani wao kama Arsenal ambao wamemaliza katika nafasi ya tano – juu yao, lakini wamekwama UCL na wanakwenda Europa huku Man U wakienda UCL.
 Ni mbinu tu na ujanja lakini vina mwisho. Lazima Mourinho ahakikishe anajijenga vyema na kikosi chake, maana ukiangalia tangu mwanzo wa msimu, akiwa na wachezaji wazuri, mahiri, ghali kwenye kila eneo kuanzia golikipa, hawakufanya vyema, wakafungwa kisha wakaendekeza sare nyingi.
Ukiachilia mbali kombe hilo na kufuzu kwao, kuna maswali mengi kuliko majibu juu ya kipi kikosi hicho kilifanya kwenye EPL; kulikoni mkusanyiko wa kikosi aghali jinsi hiyo ushindwe kufanya mambo kiasi cha kuzidiwa kwenye nafasi na hao niliowataja awali.
Je, Mourinho anaishiwa mbinu za kufundisha na kuishia kuegesha basi ili kuona kwamba wanakwenda sare nyingi vile? Kwenye fainali ile dhidi ya vijana wadogo kabisa wa Ajax, United walikuwa ndicho kikosi ghali zaidi kupata kucheza kwenye fainali ya Europa, lakini shangaa kwamba Marouane Fellaini eti ndiye alichezeshwa kama mshambuliaji pekee.
Kama ni kiu, basi Mourinho alikuwa nayo ya kupata kikombe msimu huu, na moyo wake haukutulia hadi alipojihakikishia kwamba amepata hicho; bao la kwanza lilipofungwa hakushangilia, akijidai kwamba ama hakuona au alikuwa na mawazo mengine.
Lakini lilipofungwa lile la pili, alisimama na kushangilia na mwonekano wa tangu hapo uliashiria kitu kimoja – gemu ilikuwa imeisha na ushindi ni wake. Hata kitendo chake cha kulibusu kombe kabla halijakabidhiwa kwa nahodha Wayne Rooney na kisha kujidai kutoroka nalo ilikuwa ni ishara tosha kabisa jinsi lilivyomaanisha makubwa kwake.
Naam, katika majenzi mapya ya klabu hiyo ambayo haijapata kuwa juu tangu kuondoka kwa kocha mkongwe Alex Ferguson, ilikuwa muhimu kushinda – kufuzu kwa UCL, lakini njia aliyopitia kwa sasa inaweza kupuuzwa, japokuwa msimu ujao ataangaliwa kwa jicho yakinifu zaidi.
Mourinho alipingwa na wengi kwa njia aliyopitia, lakini akawaambia wapinzani hao wa ndani na nje  ya klabu watulie kimya na Jumatano hii aliwaonesha kwa nini alikuwa akifanya hayo – anaenda UCL na wakubwa zao kimsimamo – Arsenal, wanakwenda kwenye ligi ndogo na ngumu, inayohusisha mechi nyingi na safari za mbali, michosho kwa wachezaji na pengine kuumia, ikizingatiwa Arsenal wamekuwa na kikosi cha wachezaji wanaoumia hovyo hovyo.

No comments:

Post a Comment