LIGI Daraja la kwanza inatarajiwa
kuendelea kesho kwenye viwanja tisa tofauti, huku Lipuli ikitarajiwa kutangaza
kupanda Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao.
Akizungumza na gazeti hili, Mtendaji
Mkuu wa Bodi ya Ligi, Boniface Wambura alisema timu 18 zinatarajiwa kushuka
uwanjani katika miji tisa tofauti.
Vinara wa Kundi A Lipuli ambao
wanatafuta pointi moja kujihakikishia kupanda ligi kuu msimu ujao itaialika
Polisi Dar, Kiluvya itacheza na Pamba, Friends Ranger itakuwa mwenyeji wa African
Sports mchezo utakaochezwa Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.
Kundi B Polisi Moro itakuwa mwenyeji
wa KMC kwenye Uwanja wa Jamhuri,mchezo ambao utaamua nani awe juu ya mwenzake
kwani wote wana pointi 19.
Coastal Union itaialika Mlale JKT
kwenye Uwanja wa Mkwakwani Tanga, Mbeya Warriors itacheza na vinara wa kundi B
Njombe Mji yenye pointi 21.
Kundi C Polisi Mara itacheza na
vinara Singida Utd yenye pointi 26, Mvuvumwa itacheza na Alliance yenye pointi
23 kwenye nafasi ya pili na Rhino Rangers ambayo inashika nafasi ya tatu ikiwa
na pointi 21 itacheza na Polisi Dodoma.
Jumapili Mgambo Shooting itacheza na Panone
kwenye Uwanja wa Mkwakwani na Ashanti
itacheza na Mshikamano kwenye Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment