Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Wednesday, October 19, 2016

BARAZA LA WAZEE YANGA LASEMA YANGA SIYO MAFURIA YA SHUGHULINI IKODISHWE


BARAZA la wazee wa Yanga limesema timu hiyo haiwezi kukodishwa kama masufuria ya shughulini kwa namna yoyote ile kutokana na historia iliyonayo tangu kuanzishwa kwake mwaka 1935.

Yanga inaelekea kwenye mkutano mkuu wa dharura utakaofanyika Jumapili ijayo Oktoba 23 ambapo miongoni mwa Ajenda zitakazojadiliwa ni pamoja na suala la kukodishwa huku kampuni ya Yanga Yetu iliyo chini ya Mwenyekiti Yusuph Manji ikiwa na nia ya dhati ya kuikodisha nembo ya mabingwa hao wa kihistoria.

Katibu mkuu wa Baraza hilo Mzee Ibrahim Akilimali amewaambia waandishi wa habari kuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo amekuwa akiiendesha timu kibabe ambapo sasa ameamua kutaka kujimilikisha ili iwe mali yake kitu ambacho hakitaweza kutokea kamwe.

Mzee Akilimali alisema kuwa Yanga ilivunja katiba yake kwa kukubali kumuongeza muda wa kuendelea kukaa madarakani Mwenyekiti huyo kwa mwaka mmoja kutokana na mapenzi makubwa waliyokuwa nayo na kumuamini kuwa anaweza kuivusha kumbe alikuwa na nia ya kujimilikisha timu hiyo iwe mali yake.

"Sisi Baraza la wazee msimamo wetu ni kwamba hatuko tayari kuona timu yetu ikikodishwa kama sufuria la shughuli. Tunapinga suala hilo kwa nguvu zote na halitokuja kutokea kamwe," alisema Mzee Akilimali.

Kwa upande wake Mohamed Msumi ambaye alifutwa uanachama kwenye mkutano wa dharura uliofanyika Juni  6 alisema Manji na Fransis Kifukwe ndiyo wanaoiharibu Yanga kwa ajili ya maslahi binafsi ya kutaka kujimilikisha timu hiyo kutokana na pesa walizokuwa nazo kitu ambacho watakipigania hadi mwisho.

"Manji anasema timu inadaiwa bilioni 11 tunataka atuambie tunadaiwa na nani, tulikopa kitu gani na matumizi ya pesa hizo nani aliidhinisha na kwa makubaliano ya nani akitujibu hilo ndo tutajua tufanye nini," alihoji Msumi.

Na aliyekuwa Mwanasheria wa klabu hiyo ambaye ajira yake ilisitishwa mwezi Februari mwaka huu Frank Chacha alisema mchakato wote wa kutaka kukodisha klabu hiyo ni batili kwakua umekiuka katiba ya Yanga kuanzia mkutano mkuu uliofanyika Juni 6 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee.

Chacha alisema hata Bodi ya wadhamini iliyosaini mkataba na Kampuni ya Yanga Yetu haipo kwa mujibu wa katiba ya klabu hiyo na haikusajiliwa Rita kwahiyo haina mamlaka ya kufanya jambo hilo kubwa kwa maslahi mapana ya Yanga

No comments:

Post a Comment