Kampuni ya MultiChoice Tanzania imesaini mkataba wa mwaka mmoja na mwanariadha Alphonce Felix Simbu aliyeshiriki mashindano ya Olympic ya Rio 2016 yaliyomalizika hivi karibuni huko nchini Brazil na kushika nafasi ya 5 kati ya wanariadha 157 kwenye mbio za Marathon za wanaume.
Katika Mkataba huu, Kampuni ya Multichoice Tanzania imemzawadia Alphonce Simbu shillingi za Kitanzania 1,000,0000 ambazo atalipwa kila mwezi kwa kipindi cha mwaka mmoja lengo likiwa ni kumsadia katika maandalizi yake ya mashindano yajayo ya IAAF WORLD CHAMPIONSHIP yanayotarajiwa kufanyika mjini London Uingereza August 2017.
Vile vile bwana Alphonce Simbu atapatiwa vifaa maalumu vya kuumuwezesha kufanya mazoezi yake vyema. Vifaa hivi ni kama vile, viatu na nguo za mchezo wa Riadha.
DSC_0425
Mwanariadha aliyeshiriki mashindano ya Olympic ya Rio 2016, Alphonce Felix Simbu akisaini mkataba na Kampuni ya Multichoice Tanzania. Kulia anayeshuhudia tukio hilo ni Mkurugenzi Mkuu wa Multichoice Tanzania, Maharage Chande.
Si hivyo tu bali  Kampuni ya MultiChoice itamtengenezea makala yenye kuonyesha matukio mbalimbali aliyopitia ya Kimichezo na Familia siku za nyuma. Vile vile watarekodi mazoezi atakayofanya akiwa katika kambi ya riadha Chuo cha Wakala wa Mistu Fiti kilichopo West Kilimanjaro eneo la Ngarenairobi Wilaya ya Sia Mkoa Kilimanjaro. Makala hii itarushwa kwenye DStv hapo baadae.
Katika Kipindi hicho cha mkataba huu Alphonce Felix Simbu atakuwa Balozi wa Kampuni ya MultiChoice Tanzania ambapo atashiriki katika promosheni mbalimbali kutangaza huduma zake.
Alipokuwa akisaini mkataba huo Mkurugenzi Mkuu wa Multichoice Tanzania, Maharage Chande mbele ya Rais wa Riadha Tanzania na Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Mh. Anthony Mtaka, mwalimu wake Alphonce Nd. Francis John Marcially pamoja na Meneja Masoko wa MultiChoice Tanzania, Furaha Samalu, alisisitiza kuwa “huu ni mwanzo na kadri mafanikio yanavyoongezeka Multichoice itakuwa tayari kuwa mstari wa mbele kushirikiana na chama cha riadha Tanzania katika kunyanyua riadha Tanzania na kurudisha heshima ya taifa kwenye mchezo huo”.
DSC_0432
Mkurugenzi Mkuu wa Multichoice Tanzania, Maharage Chande (wa pili kulia aliyeketi) akimkabidhi nakala ya mkataba Mwanariadha aliyeshiriki mashindano ya Olympic ya Rio 2016, Alphonce Felix Simbu. Wengine katika picha ni Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Mh. Anthony Mtaka (kushoto) na Meneja Masoko wa MultiChoice Tanzania, Furaha Samalu.