Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Saturday, January 30, 2016

SIMBA YATAKATA TAIFA HUKU YANGA IKIFUNGWA MKWAKWANI






SIMBA leo imezidi kuwapa raha mashabiki wake baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya African Sports Uwanja wa Taifa Dar es Salaam, huku Yanga ikilala mabao 2-0 mbele ya Coastal Union Uwanja wa Mkwakwani Tanga.

Ushindi wa Simba ulipokelewa kwa furaha kubwa na mashabiki wa timu hiyo na umeifanya iendeleze rekodi nzuri ya ushindi katika mechi zake tatu mfululizo sasa


Wiki za hivi karibuni Simba ilimuondoa kocha wake Dylan Kerr na kocha wa makipa, Iddi Salim kwa kilichoelezwa timu haichezi vizuri na jukumu kukabidhiwa Mganda Jackson Mayanja, ambaye alikuwa Kocha Msaidizi.


Huo ni ushindi wa pili mfululizo kwa Simba katika ligi hiyo ikiwa chi ya Mayanja baada ya mchezo wa kwanza kuifunga Mtibwa Sugar bao 1-0 wiki mbili zilizopita, lakini ni wa tatu mfululizo kwa kocha huyo baada ya Jumamosi wiki iliyopita kuifunga Burkina Faso mabao 3-0 iliyopo Ligi Daraja la Kwanza katika kuwania Kombe la Shirikisho Uwanja wa jamhuri Morogoro.


Kutokana na ushindi huo wa jana, Simba sasa imefikisha pointi 36 ikiendelea kushika nafasi ya tatu nyuma ya Azam inayoshika nafasi ya pili ikiwa na pointi 39 na Yanga inayoongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 39, lakini ina uwiano mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa. Azam ipo nyuma mchezo mmoja.


Katika mchezo wa jana, Simba ilipata bao la kwanza dakika ya 14 mfungaji akiwa Hamisi Kiiza akimalizia krosi ya Hassan Ramadhan Kessy, kabla ya Kessy kuifungia Simba bao la pili dakika ya 30 baada ya kuwalamba chenga mabeki wa African Sports.


Simba iliendelea kufanya mashambulizi ya nguvu, huku Sports wakionekana kuzidiwa kila idara, ambapo dakika ya 42 Kiiza alifunga bao la tatu kutokana na uzembe wa beki Halfan Twenye aliyerudisha mpira kwa kipa wake  na Kiiza kuunasa.

Bao hilo la Kiiza lilikuwa la 12 kwake kufunga katika msimu huu akiendelea kuwa nyuma ya Amis Tambwe wa Yanga anayeongoza akiwa na mabao 13.


Sports ilijaribu mara chache kufurukuta, lakini umaliziaji haukuwa mzuri, ambapo wachezaji Pera Ramadhan na Rajabu Isihaka walishindwa kuzitumia.

Simba iliongeza bao la nne dakika ya 75 mfungaji akiwa Haji Ugando baada ya kupokea pasi ya Kessy na kuibua shangwe kwa mashabiki wa timu hiyo.


Wakati huohuo, Yanga jana ilipoteza mchezo wa kwanza katika ligi ya msimu huu baada ya kupokea kipigo cha mabao 2-0 Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Yanga na Azam zilikuwa ndiyo timu pekee katika ligi hiyo msimu huu, ambazo hazifungwa mechi, hivyo kwa matokeo hayo imebaki Azam pekee.


Coastal ilipata bao la kwanza dakika ya 27 mfungaji akiwa Miraji Adamu kwa mpira wa adhabu baada ya beki Kelvin Yondani kuunawa mpira na kupiga adhabu hiyo iliyomshinda kipa Deogratias Munishi ‘Dida’.

Washambuliaji wa Yanga wakiongozwa na Donald Ngoma walijaribu kufukuta kutaka kusawazisha bao hilo, lakini umaliziaji ulikuwa butu.

Dakika ya 62, Juma Mahadhi alifunga bao la pili kwa shuti kali, bao ambalo liliwaamsha mashabiki wa Coastal, ambao matokeo hayo yamewafanya wafikishe pointi 13.

Naye Alexander Sanga anaripoti kutoka Shinyanga kuwa Mwadui imeibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Toto Aficans mchezo uliofanyika Uwanja wa Mwadui.Bao hilo lilifungwa dakika ya 63 na Kelvin Kongwe kwa shuti la mbali.

Hicho ni kipigo cha nne mfululizo kwa Toto Africans baada ya kufungwa na African Sports, Prisons na Stand United.

Mchezo mwingine uliofanyika Uwanja wa Karume, Dar es Salaam, ambapo JKT Ruvu na Majimaji zilitoka 0-0.


 

No comments:

Post a Comment