Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Friday, February 7, 2014

MALINZI AZUNGUMZA NA WAANDISHI WA HABARI LEO KUHUSU SIKU 100 TANGU AINGIE MADARAKANI, SOMA TAARIFA YAKE

Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Jamali Malinzi (katikati) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari jana kuhusu siku 100 tangu walipoingia madarakani. Kulia ni msaidizi wa Rais masuala ya Ufundi, Pelegrinius Rutahyuga na kushoto ni Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura.



Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi ameelezea hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa Ilani yake siku 100 tangu alipoingia madarakani.



Akizungumza na waandishi wa habari leo (Februari 7 mwaka huu) katika mkutano uliofanyika katika hoteli ya Hyatt Regency jijini Dar es Salaam, Rais Malinzi aliainisha maeneo kadhaa yaliyopewa kipaumbele na tayari yameanza kufanyiwa kazi pamoja na changamoto zilizopo.



Alisema muundo wa Idara ya Ufundi umebadilishwa kwa kuundwa vitengo vya ufundi, elimu na maendeleo ya mpira wa miguu huku maeneo ambayo tayari yameanza kufanyiwa kazi kuwa ni;



Ujenzi wa kituo cha mpira wa miguu (football centre of excellency), timu kupanda daraja, kuanzisha mashindano mapya na kufufua ya zamani, mpira wa miguu wa wanawake, maandalizi ya vijana (grassroot football), tiba, walimu na makocha, utawala, uhusiano na Zanzibar, klabu za mpira wa miguu, wachezaji, masoko na uwekezaji, kitengo cha habari, viwanja na timu ya Taifa (Taifa Stars).



Rais Malinzi amesema changamoto zilizopo kwa sasa ni matumizi ya tiketi za elektroniki, ufinyu wa bajeti, madeni, nidhamu, maadili na uchezeshaji wa waamuzi.



Ametoa mwito kwa wadau wote nchini wakiongozwa na Serikali, Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Afrika (CAF), Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), vyombo vya habari, mashirika ya umma na kampuni binafsi kushikamana na kuwa kitu kimoja kwa nia ya kuinua kiwango cha mpira wa miguu Tanzania.





TANZANIA  FOOTBALL  FEDERATION


TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA ILANI YA UCHAGUZI
YA RAIS WA TFF


Ndugu zangu,

Uchaguzi mkuu wa TFF ulifanyika tarehe 27 Oktoba, 2013 na kukamilika alfajiri ya tarehe 28 Oktoba, 2013 ambapo Kamati ya Utendaji ya TFF ilitangazwa rasmi na aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi wa TFF Ndugu Hamidu Mbwezeleni.

Katika kuelekea uchaguzi mkuu huo niliitisha mkutano na waandishi wa habari ambapo nilitangaza ilani yangu ya uchaguzi.  Lengo la ilani ilikuwa ni kuwaeleza wadau na wapenzi wa mpira wa miguu Tanzania dira ambayo ingeongoza mpira wetu iwapo ningechaguliwa kuwa Rais wa TFF.  Aidha niliahidi iwapo ningechaguliwa tungekutana katika chumba hiki hiki  baada ya siku 100.  Ninapenda nichukue fursa hii  kuwashukuru na kuwapongeza wajumbe wote wa Mkutano Mkuu wa TFF, walionipa kura na ambao hawakunipa kura, kwa kukamilisha vyema zoezi la uchaguzi huo.  Uchaguzi umekamilika kazi iliyobakia mbele yetu ni kutekeleza majukumu yetu kama viongozi wa mpira miguu Tanzania.

Ilani na Utekelezaji wake

Ilani yangu ya uchaguzi iliainisha maeneo kadhaa ya kupewa vipaumbele.  Nitakumbushia maeneo haya na kueleza hatua tulizofikia katika utekelezaji wake:

1.            Idara ya Ufundi
1.1              Kikao cha Kamati ya Utendaji kilichokaa tarehe 23 Novemba, 2013 pamoja na mambo mengine kilipitisha muundo mpya wa Sekretariati ya TFF.  Muundo huo unaelezwa katika chati hii hapa chini:








 











                                                                                                           
                                                                                                                                                                Commercial Manager




General Secretary
 
 


                         
                                Media Officer                                                                                                  Chief Security Officer













 








Katika muundo huu  Idara ya Ufundi imepanuliwa kwa kuundwa vitengo vya Ufundi,Elimu na Maendeleo ya mpira.
Aidha katika kutekeleza azma ya kuboresha usimamizi wa mpira wa vijana (Youth Football) Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania limeamua kuajiri Desk Officer wa vijana yaani msimamizi maalum wa mpira wa vijana na tayari ameajiriwa.
Zoezi la kuimarisha Idara ya Ufundi kwa kuajiri Mkurugenzi wa Ufundi pamoja na Wakurugenzi wake Wasaidizi linaendelea.


1.2              Ujenzi wa Kituo cha Mpira (Football Centre of Excellency)

Limekuwa ni jambo la kufurahisha na kutia moyo kuwa mara baada ya kuingia madarakani Serikali kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ilitufahamisha juu ya uamuzi wa Serikali, kwa kushirikiana na Kampuni ya SYMBION ya Marekani na Klabu ya Mpira ya SUNDERLAND ya Uingereza, wa kujenga kituo cha michezo (Sports Centre) Kidongo Chekundu , Ilala na kujenga kituo cha kulea na kukuza vipaji vya vijana (Elite Academy) Wilayani Kinondoni.  Wizara ilinikutanisha na Uongozi wa SYMBION na mazungumzo yanaendela kuona ni jinsi gani mradi huu utashirikisha Serikali, Mshirika wetu SYMBION, Klabu ya SUNDERLAND na TFF ambao kwa mujibu wa katiba yetu  ndio waratibu na wasimamizi wa maendeleo ya mpira wa miguu Tanzania.  Vikao kadhaa vimefanyika na mwelekeo ni mzuri sana.  Tunaamini mradi huu utatoa mchango mkubwa sana katika kuendeleza mpira wa vijana (Youth Football).
Aidha kamati ya utendaji ya TFF imeviagiza vyama vyote vya mpira vya mikoa kuomba kumilikishwa viwanja vikubwa katika  maeneo mapya yanayopimwa, TFF italipia malipo yote yatakayotakiwa. Mkoa wa Tanga tayari wametekeleza agizo hili na hati imekwisha toka.Msanifu tayari anaanda michoro ya awali kwa ajili ya kujenga kituo cha michezo katika ardhi hii. Mfano wa mchoro wa kituo hiki ndio utakaotumika nchi nzima iwapo utapitishwa na kamati ya utendaji.

1.3              Timu Kupanda Daraja

TFF tayari imeunda Kamati ya dharura (Adhoc) ya kuangalia mapungufu yaliyopo katika utaratibu wa sasa wa kuwa na timu 14 za Ligi Kuu na 24 za Ligi Daraja la Kwanza ili tuone ni kwa jinsi gani tutaweza kuboresha Ligi yetu.  Ripoti ya Kamati ikikamilika italetwa mbele ya Kamati ya Utendaji kwa ajili ya maamuzi ya mwisho.

1.4              Kuanzisha Mashindano Mapya na Kufufua ya Zamani

Juhudi zinaendelea kuhakikisha mashindano ya Kombe la Taifa yanafufuliwa.  Aidha taratibu za kuanzisha upya Kombe la Shirikisho (Federation Cup) ambalo litakuwa ni la mtoano nchi nzima  zimefikia hatua nzuri na muda si mrefu taratibu zake zitatangazwa pindi mshirika wetu atakapokuwa amemaliza maandalizi upande wake.

1.5              Mpira wa Wanawake

1.5.1        Katika kuhakikisha mpira wa wanawake unatengenezwa mkakati maalum wa maendeleo matayarisho ya mpango wa maendeleo ya mpira wa wanawake (women football development plan) yamekamilika na yatawasilishwa katika kikao kijacho cha Kamati ya Utendaji kwa ajili ya maamuzi ya mwisho.  Mpango huu utatoa dira ya maendeleo ya mpira wa miguu kwa miaka mitano ijayo na utakuwa ni  sehemu ya mpango kazi wa TFF wa miaka mitano.

1.5.2        TFF inayo furaha pia kuufahamisha umma wa wapenda mpira wa Tanzania kuwa shula ya kukuza na kuendeleza vipaji ya Alliance Mwanza kwa kutambua mapungufu yaliyopo katika kuendeleza mpira wa wanawake kuanzia mwaka huu imeanzisha mafunzo maalum ya mpira wa watoto wa kike umri chini ya miaka 10.  Matunda yake tutayaona baadaye. Hawa watakuzwa na kulelewa pamoja.

1.5.3        Jitihada zinafanyika kuanza mashindano ya kitaifa ya wanawake na muda si mrefu utaratibu wake utatangazwa baada ya mshirika wetu kumaliza maandalizi yake.

1.5.4        TFF kwa kushirikiana na Wizara ya Wanawake na  Jinsia ipo katika kuandaa mpango kazi wa kushirikiana na vyuo 55 vya Ustawi wa Jamii Tanzania katika kuanzisha masomo maalum kwa wasichana katika vyuo nchini, masomo ambayo yatahusisha ufundishaji wa mpira wa wanawake, urefa, ukocha na utawala wa mpira.  Lengo ni kutoa fursa kwa wasichana kujifunza stadi hizi kama sehemu ya masomo yao katika vyuo vya maendeleo ya jamii.  Utaratibu wa mpango huu unasimamiwa na chama cha mpira wa migu wa wanawake (TWFA) na taasisi nyingine husika.

1.5.5        Pamoja na ufinyu wa bajeti tulionao na timu zetu za wanawake kutokuwa na udhamini TFF bado inahakikisha timu zetu za wanawake zinashiriki michuano yote ya kimataifa.Wiki iliyopita timu yetu ya Taifa ya wanawake imesajiliwa kushiriki mtoano wa kushiriki fainali za All Africa games Congo Brazzavile 2015.

1.6              Maandalizi ya Vijana  (Grassroot Football)

Mpango kazi wa maendeleo ya mpira wa miguu wa vijana  Tanzania (Tanzania youth development plan)  maandalizi yake yamekamilika na utazinduliwa muda si mrefu.   Vipaumbele vikuu vya mpango huu ni pamoja na:

1.6.1        Kuhakikisha shule zote za msingi 16,000 za  Tanzania   zinakuwa na viwanja vya kuchezea mpira, mwalimu mmoja wa mpira na zinapata   kwa mwaka angalau mipira 10 ya size 3 na 4 pamoja na jozi angalau 30 za viatu.

TFF tayari inawasiliana na Mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali ili yatukusanyie vifaa vya mpira vilivyotumika (has viatu) ili viweze kuletwa na kugawiwa kwa watoto wetu kwenye shule za msingi na academies.  Kwa sasa tayari kontena mbili za vifaa hivi zimekwisha  kusanywa nchini Uingereza na utaratibu wa kuzileta unafanyika.  Lengo ni kuingiza nchini jozi za viatu 500,000 kwa mwaka na mipira 160,000 ya size 3 na 4 kwa mwaka.  TFF inaomba ushirikiano wa Serikalini, Taasisi za Umma, Makampuni Binafsi na Taasisi zisizo za kiserikali katika kuhitimisha azma hii.

1.6.2        TFF ilipata fursa ya kukutana na Balozi wa Uholanzi hapa nchini na kufanya naye mazungumzo.  Nia na lengo ilikuwa ni kuangalia ni kwa jinsi gani Uholanzi inaweza kutusaidia kufundisha walimu wa walimu (trainer of trainers).  Matumaini yetu ni kuwa walimu hawa wakishafuzu watakuwa na  jukumu la kuwafundisha walimu wa michezo wa shule za msingi kwa kushirikisha vyuo vya walimu vinavyotoa taaluma hii kama Malya, Murutunguru na Butimba.

1.6.3        TFF kwa kushirikiana na taasisi isiyo ya kiserikali inaangalia uwezekano wa kujenga vituo vya michezo 169 katika Wilaya zote 169 Tanzania.  Vituo hivi pamoja na kufundisha mpira vitakuwa pia ni vituo maalum vya kuwafundisha vijana juu ya athari za matumizi ya dawa za kulevya.

1.6.4        TFF kupitia Idara yake ya Ufundi na Kamati ya Vijana iko mbioni kufanya sensa ya vituo vya kukuza na kulea vipaji vya vijana (Academies) pamoja na vituo vya mpira (Sports Centres) nchini kote Tanzania.  Utaratibu unafanywa wa kuweka vigezo vya kutambuliwa vituo hivi na TFF itaanzisha utaratibu wa kusajili na kutoa vyeti vya usajili kwa vituo vitakavyokidhi vigezo.  Lengo ni kuweka utaratibu nchini wa kusimamia na kuendeleza vituo hivi kitaifa.

1.6.5        Mpango wa muda mfupi wa TFF ni kuandaa timu ya Taifa ya vijana itakayoshiriki mashindano ya Fainali za Afrika umri chini ya miaka 17 mwaka 2019.  Tanzania tumeomba uenyeji wa Fainali hizi.  Mwaka huu wa 2014 TFF itafanya mashindano maalum ya vijana chini ya umri wa miaka 12 ili kuunda timu ya Taifa ya kuanzia ya U12, timu ambayo itakua pamoja kuelekea 2019.  Malengo ni kuiboresha timu hii kila mwaka kwa kuongeza vijana U13 mwaka 2015, U14 mwaka 2016, U15 mwaka 2017 na mwishowe U16 mwaka 2018.TFF imekwisha pata mshirika wa mpango huu na akimaliza maandalizi yake atatangazwa rasmi.

1.6.6        Ili Tanzania ifundishe mpira unaofanana nchini kote, utaratibu unafanyika wa kuandaa mtaala wa kufundisha mpira (National football curricullum).  Mtaala huu unaandaliwa na Idara ya Ufundi ya TFF kwa kusaidiana na Mtaalam wa mpira toka Uholanzi.  Mtaala huu ukikamilika utakuwa nyenzo muhimu ya kufundishia mpira mashuleni na kwenye Academies.

1.7              Tiba, Waalimu na Makocha

TFF imeandaa mpango wa kukutana na wenyeviti wa vyama vya Tiba, Waamuzi na Makocha ili kupanga nao mikakati ya maendeleo ya kitaaluma.  Mikakati hii ikiwa tayari itajumuishwa katika mpango mama  wa maendeleo wa TFF (TFF National Business Plan), mpango ambao maandalizi yake yatakamilika ndani ya miezi  mitatu kuanzia sasa.

1.8         Utawala

TFF imeanza kwa kuboresha mazingara ya utendaji wa kazi.  Vyama shiriki TAFCA, FRAT, TASMA, TWFA na SPUTANZA tayari vimepatiwa ofisi za kisasa katika eneo la Ilala.  Ofisi kuu za TFF nazo ziko mbioni kuhamia katika jengo la kisasa la PPF Tower,nia ikiwa ni kuiwekea sekretariet ya TFF mazingira ya kisasa ya kufanyia kazi na pia kupisha ujenzi wa kitega uchumi eneo letu la Uwanja wa Karume.

Aidha TFF imeunda kamati maalum (Adhoc) ya kupitia Muundo wa Bodi ya Ligi lengo likiwa ni kutekeleza maagizo ya Mkutano Mkuu wa TFF ulioagiza Bodi ya Ligi iundwe ikiwa ni ya mpito kuelekea uundwaji wa Kampuni ya kuendesha Ligi Kuu ya mpira wa miguu.

1.9         Mahusiano na Zanzibar

Mahusiano kati ya TFF na Chama cha mpira Zanzibar (ZFA) yamezidi kuimarishwa kufuatia ziara kadhaa ambazo tumezifanya kati ya maeneo yetu mawili.  Mipango ya kuimarisha timu zetu za Taifa za wakubwa, za vijana na za wanawake inafanywa kwa pamoja.  Juhudi za kuhakikisha Zanzibar inajiunga na FIFA pia zinaendelea kupitia mazungumzo na wahusika.

1.10       Vilabu vya Mpira

                Mara baada ya kuingia madarakani Uongozi wa TFF ulikutana na viongozi wa vilabu vyote vya Ligi Kuu na Ligi Daraja la Kwanza.  Kikao hiki kilifanyika kama sehemu ya kuangalia ni maboresho gani yafanyike ili kuongeza ufanisi katika uendeshaji wa Ligi zetu.  Utekelezaji wa maazimio ya kikao hicho unaendelea kupitia wahusika mbalimbali.

1.11       Wachezaji

                SPUTANZA wameleta TFF mapendekezo yao ya jinsi ya kuboresha maslahi ya wachezaji wa mpira wawapo mpirani na baada ya kustaafu kucheza soka.  TFF inayafanyia kazi mapendekezo hayo.  Lakini kubwa litakuwa ni kuanzisha Mfuko Maalum (Trust Fund) utakaochangiwa na wachezaji wakiwa bado wanacheza pamoja na TFF na taasisi nyingine ili mfuko huu uwasaidie pindi wakistaafu.




1.12       Masoko na Uwekezaji

                Kama nilivyoeleza hapo juu TFF iko mbioni kuwekeza katika Kiwanja cha Karume, lakni pia njia nyingine za kuiongezea TFF mapato ziko mbioni kuanzishwa ikiwa ni pamoja na kuanzisha utaratibu maalum wa kuuza jezi za Timu ya Taifa (replica shirts).

1.13       Kitengo cha Habari

                TFF imeandaa utaratibu wa kuboresha kitengo hiki kwa kukiongezea nguvu kazi ili upashanaji wa habari uwe ni wa haraka zaidi ikiwa ni pamoja na TFF kuanzisha Blog  yake,kuboresha Tovuti yake, na kuwa na kurasa kwenye mitandao ya kijamii kama Instagram, Facebook, Twitter, n.k. Press officer ataajiriwa punde ili kuimarisha kitengo hiki.

1.14       Viwanja

                Wakati tunaingia madarakani FIFA kupitia mpango wake wa maendeleo ilikuwa imekwisha  tenga pesa kwa ajili ya kuweza nyasi bandia uwanja wa kihistora wa Nyamagana  jijini Mwanza.  Uongozi wetu kwa kushirikiana na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo pamoja na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza na Meya wa Manispaa ya Mwanza tulifuatilia kwa karibu na kufanikiwa kuondoa dosari zilizokuwa zimekwamisha mradi huu.  Utandazaji wa nyasi bandia utaanza mara moja kuanzia sasa.

                Kwa mafanikio haya Tanzania tuna viwanja vyenye/ vitakavyokuwa na nyasi bandia baadae ambavyo ni Gombani Pemba, Amani Zanzibar,Uwanja wa Uhuru, Uwanja wa Karume, Uwanja wa Azam Chamazi na Uwanja wa Nyamagana.

                TFF iko mbioni kuanza mazungumzo na baadhi ya vyama vya siasa ambavyo ni wamiliki wa viwanja kadhaa vya mpira ili kuangalia uwezekano wa kuingia ubia kwa nia ya kuviendeleza.



1.15       Timu ya Taifa (Taifa Stars)

                Ili kuandaa mkakati maalum wa kuboresha timu ya Taifa TFF iliitisha kikao maalum cha walimu wa mpira waandamizi.  Kikao hiki kilifanyika Zanzibar kati ya tarehe 06-07 Desemba, 2013 na kilitoka na maamuzi kadhaa.  Tarehe 18-19 Januari, 2014 TFF iliitisha kikao kingine maalum cha Makatibu 30 wa vyama vya mpira vya mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar ajenda ikiwa ni uboreshaji wa Timu ya Taifa (Taifa Stars). Matunda ya vikao hivi ni mpango kazi maalum ulioandaliwa  wa kuboresha timu ya Taifa kwa kushirikiana na washirika wetu Tanzania Breweries ltd kupitia bia yao ya Kilimanjaro Lager. Mpango huu utatangazwa rasmi wiki ya pili ya mwezi  February 2014.

CHANGAMOTO:
Uongozi mpya tangia umeingia madarakani umekutana na changamoto kadhaa. Baadhi yake ni kama hizi zifuatazo:
1.Tiketi za Elektronik.
Uongozi mpya ulipoingia madarakani ulikuta awamu iliyopita ilikwisha saini mkataba wa mradi huu.Jukumu la uongozi wangu ni kutekeleza masharti ya mkataba. Changamoto nyingi zimejitokeza ikiwa ni pamoja na mitambo kuzima mara kwa mara,mitambo kufanya kazi kwa spidi ndogo , mageti yaliyofungwa mashine hizi kuwa machache (mfano Mkwakwani yamefungwa mitambo miwili katika uwanja unaoingiza watu zaidi ya elfu kumi,uwanja wa Taifa mitambo 48 wakati unaingiza watu 60,000,linganisha na uwanja wa Emirates London unaoingiza watu 60,000 mitambo imefungwa 125,karibia mara tatu ya uwanja wetu wa Taifa). Pia uelewa mdogo wa wadau kuhusu taratibu za utumiaji tiketi hizi nao ni tatizo na mkataba wa TFF na CRDB unaitaka TFF ibebe jukumu la kutoa elimu kwa umma kuhusu matumizi ya tiketi hizi  na bajeti yake haipungui shilingi milioni 500 ikijumuisha gharama za matangazo kwenye radio,magazeti,televisheni,roadshows,mabango,vipeperushi n.k. Matokeo yake yalikuwa ni vurugu katika baadhi ya viwanja, vurugu ambazo kama si busara za TFF zingeweza kusababisha maafa.Mazungumzo yanaendelea kati ya TFF na mzabuni CRDB ili  kutafuta namna ya kuboresha utaratibu wa mfumo wa tiketi za elektronik,lakini pia ni kuangalia ni kwa jinsi gani tiketi hizi hazigeuki kuwa mzigo kwa mlaji maana licha ya watazamaji kulipia gharama ya tiketi yenyewe lakini bado kuna asilimia inakatwa kama kamisheni ya uwakala jambo ambalo pia ni mzigo kwa vilabu.TFF ina nia thabiti ya kutumia utaratibu huu,ni mzuri iwapo utatekelezwa kwa taratibu stahili.


  1. Ufinyu wa bajeti
TFF katika kutimiza majukumu yake inahitaji pesa nyingi hasa kuendeleza mpira wa vijana, kukidhi gharama za kuendesha ofisi, kuvipa nguvu vyama wanachama na kusimamia timu zake nane za Taifa (Za wakubwa mbili wanawake/wanaume,U17 mbili,U20 mbili na za olimpiki mbili).Eneo lenye ufadhili mkubwa ni timu ya Taifa ya wanaume tu.Hivyo ni dhahiri mahitaji ya fedha TFF ni makubwa sana na vyanzo havikidhi.Jitihada zinafanyika kuhakikisha tunaongeza vyanzo mbadala wa mapato.
  1. Madeni
Madeni ambayo uongozi mpya ulipoingia madarakani uliyakuta ni makubwa na yamelielemea shirikisho. Juhudi za kuongea na wanaotudai ili aidha watupunguzie madai yao au tuyalipe kwa masharti nafuu yanaendelea.Wale wote wanaotudai ambao wametuelewa katika hili tunawashukuru sana. Kwa sasa kesi zote za madai dhidi ya TFF  zilizokuwa mahakamani zimeondolewa baada ya mapatano.
  1. Nidhamu
Nidhamu bado ni tatizo si kwa wachezaji bali hata kwa viongozi wetu.Yupo mchezaji amediriki kupigana na walinzi wa raia na wengine wakadiriki kumpiga mwamuzi,hili halikubaliki na hatua kali zitakuwa zinatolewa dhidi ya watovu wa nidhamu bila kujali wao ni kina nani kwenye mpira wa nchi hii.
  1. Maadili
Wizi mdogo mdogo hasa wa mapato ya milangoni umeendelea.TFF tumekuta kesi za wizi wa aina hii zaidi ya hamsini zilizoripotiwa polisi Chang’ombe na watuhumiwa hawakuwahi kupelekwa mahakamani kwa kuwa mlalamikaji (TFF) hakujitokeza kuandika taarifa (statement). Uongozi wangu umeamua utakuwa unafuatilia kwa karibu kesi hizi ili kukomesha tabia iliyozoeleka ya udokozi.Pesa ya mpira itumike kwenye mpira.
  1. Maamuzi uwanjani (Refeering)
Wapo waamuzi wanaokosea kwa makosa ya kibanadamu, hao tunawaelewa.Lakini zinapotokea tetesi au tuhuma za haki kutotendeka kiwanjani kwa sababu nyingine zaidi ya hii shirikisho linashtuka sana na kamwe halitakubali lidhalilike kwa tuhuma kama hizi.Shirikisho kwa sasa linafuatilia kwa karibu kinachoendelea uwanjani ili kuhakikisha haki inatendeka kwa timu zote. Tayari mitihani imekwisha fanyika kupandisha madaraja waamuzi mbali mbali ili kuongeza uwigo wa kupata waamuzi.Kozi za waamuzi zitaendelea kutolewa ili kuzidi kunoa uwezo wao.
Aidha vituo vya kuendeleza waamuzi vijana vya kambi ya Jenerali Twalipo na Alliance academy Mwanza viko mbioni kuimarishwa  ili viwe na  nguvu zaidi ya kufundisha waamuzi vijana.







HITIMISHO

Ndugu zangu nihitimishe kwa kutoa wito kwa wadau wote wa Mpira wa Miguu Tanzania wakiongozwa  na Serikali, CAF, FIFA, CECAFA, vyombo vya habari, Mashirika ya Umma, Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Makampuni na watu binafsi wote kwa pamoja tushikamane kwa pamoja tukiwa na nia moja tu, kuinua kiwango cha mpira Tanzania na kuzifanya timu zetu za mpira ziwe za wakubwa, za wanawake na  za vijana ziwike, sio  tu barani Afrika, bali duniani pote.  Kwa pamoja tunaweza. 
Tukijaliwa tutakutana tena ndani ya chumba hiki hiki baada ya siku 365 tangia nimechaguliwa kuongoza TFF ili tufanye tathmini ya mwaka mmoja wa uongozi wangu. 

Mungu ibariki TFF
Mungu Ibariki Tanzania
Mungu ibariki Afrika


Jamal Malinzi
Rais wa TFF
07 Januari, 2014

No comments:

Post a Comment