Mchezaji wa Timu ya Mkoa wa Kaskazini Unguja Ame Ali mwenye mpira akitafuta mbinu za kumtoka mchezaji wa Mkoa wa Mjini katika fainali ya Dkt. Shein Cup,Kaskazini ilishinda 3-1


Timu ya Soka ya Mkoa wa Kaskazini Unguja imefanikiwa kutwaa Ubingwa wa Dkt. Shein Cup baada ya kuitandika Timu ya Mkoa wa mjini mabao 3-1 katika fainali za kuazimisha miaka 36 ya kuzaliwa CCM zilizofanyika jana Uwanja wa Amani mjini Zanzibar

Fainali hiyo ambayo mgeni rasmi alikuwa Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar zilikuwa za aina yake kutokana na wingi wa Mashabiki na Wanachama wa CCM kujitokeza katika mtanange huo.

Timu hizo zilishambuliana kwa zamu katika kipindi cha kwanza huku kila timu ikiwa inatengeneza pasi safi kwa ajili ya kujihakikishia bao la mapema jambo lililozidi kuhanikiza furaha ya mchezo huo.

Alikuwa ni Ame Ali aliyeanza kuipatia Timu yake ya Mkoa wa Kaskazini Unguja bao la kuongoza kupitia Mkwaju wa penelti mnamo dakika ya 36 lililodumu hadi kumalizika kwa kipindi cha kwanza.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kufanya mabadiliko ya wachezaji ili kuongeza nguvu lakini mabadiliko hayo yalionekana kuisaidia zaidi timu ya Kaskazini Unguja na kuweza kuutawala mchezo huo kwa kiwango kikubwa.

Mchezaji Ali Kurwa aliweza kuipatia bao timu yake ya Kaskazini dakika ya 87 kabla ya mwenzake Hilali Rihani kupachika bao la tatu dakika ya 89.

Bao pekee la kufutia machozi la timu ya Mkoa wa Mjini kichama lilipachikwa kimiani na mchezaji Hassan Juma dakika za ziada za mchezo huo.

Akitoa salamu zake Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano hayo Mohammed Raza alisema wamedhamiria kuyaboresha mashindano hayo mwakani kwa kuwashirikisha Wanawake wa mikoa yote ya Unguja na Pemba katika Mchezo wa Pete.

Aidha Raza alisema changamoto zilizojitokeza katika mashindano hayo zitapatiwa ufumbuzi ili kuyafanya mashindano hayo kuwa na mvuto zaidi kwa wanaCCM na Wazanzibari kwa ujumla.

Katika mashindano hayo Kipa wa Kaskazini Unguja Said Abdallah alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mashinano huku Hilali Rihani wa Kaskazini Unguja alichaguliwa kuwa Mfungaji bora ambapo Timu ya Kaskazini Pemba ilichaguliwa kuwa timu yenye nidhamu bora.

Washindi katika Mashindano hayo walikabidhiwa Kikombe na Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na kuahidiwa matembezi na hafla maalum itakayofanyika katika moja ya Hoteli kubwa zilizopo Zanzibar.

Kipa wa Timu ya Mkoa wa Mjini Hasan Juma Rajab akidaka mpira mkali uliopigwa na mshambuliaji machachari Ame Ali wa Timu ya Mkoa wa Kaskazini Unguja katika mchezo wa Fainali ya Dkt.Shein Cup uliofanyika uwanja wa Amani Mjini Zanzibar.


Mashabiki wa Timu ya Mkoa wa Kaskazini Unguja wakishangilia goli la tatu lililofungwa na mchezaji Hilali Rehani wa Timu ya Mkoa wa Kaskazini Unguja katika mchezo wa Fainali ya Dkt.Shein Cup uliofanyika uwanja wa Amani Mjini Zanzibar Kaskazini Unguja walishinda 3-1


Mashabiki wa Timu ya Mkoa wa Mjini wakiwa na nyuso za huzuni baada ya kuchezea kichapo cha 3-1 kutoka kwa Timu ya Mkoa wa Kaskazini Unguja katika mchezo wa Fainali ya Dkt.Shein Cup uliofanyika uwanja wa Amani Mjini Zanzibar.


Wachezaji wa Timu ya Mkoa wa Kaskazini Unguja wakishangiria goli lao la 3 katika mchezo wa Fainali ya Dkt.Shein Cup uliofanyika uwanja wa Amani Mjini Zanzibar.

Rais wa Zanzibar ambae pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Dr.Ali Mohammed Shein akimkabizi Kombe kepteni wa Timu ya Mkoa wa Kaskazini Unguja ambao ni mabingwa wa Dkt.Shein Cup huko katika uwanja wa Amani Mjini Zanzibar.
Picha zote na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.