MABINGWA wa
Tanzania Bara Yanga leo wamezidi kujichimbia kileleni baada ya kuichapa Stand
United ya Shinyanga kwa mabao 4-0 katika mchezo uliofanyika kwenye Uwanja wa
Taifa jijini Dar es Salaam.
Ushindi huo ni
mkwara tosha kwa watani zao Simba katika mbio za kuwania ubingwa wa ligi hiyo
baada ya wiki iliyopita kuwatoa kileleni.
Yanga imefikisha
pointi 49 ikiwa ni pointi nne zaidi ya Simba, ambayo kesho itacheza na Majimaji
ya Songea na hata ikishinda itakuwa nyuma kwa pointi moja.
Yanga katika
mchezo huo walipata bao la kuongoza katika dakika ya 19 lililofungwa na Donald
Ngoma kwa kichwa akiunganisha mpira wa Simon Msuva.
Baada ya kushindwa
kufunga katika dakika ya 11, Msuva alisahihisha makosa yake katika dakika ya 27
pale alipoifungia timu yake bao la pili baada ya krosi ya Ngoma.
Stand United ambao
katika mchezo wa kwanza dhidi ya mabingwa hao wa Tanzania Bara Yanga walishinda
1-0 kwenye Uwanja wa Kambarage, nusura wafunge katika dakika ya 26 wakati Jacob
Massawe aliposhindwa kuutumbukiza mpira wavuni akiwa nje ya 18.
Dakika ya 38,
Stand walikosa tena bao baada ya Seleman Selembe kuwa katika nafasi nzuri ya
kufunga, lakini alipiga mpira uliopanguliwa kifundi na kipa wa Yanga Munish
aliyeupangua kabla ya kuudaka.
Yanga waliakianza
kipindi cha pili kwa bao lililofungwa na Chirwa huku Msuva akikosa penalti
katika dakika ya 58 baada ya kupaisha mpira.
Penalti hiyo
ilitolewa baada ya Revocatus Richard kufanya madhambi ndani ya 18, lakini Msuva
alipiga shuti lililopa juu ya lango.
Mkongwe Nadir
Haroub alifunga bao la nne kwa Yanga katika dakika ya 68 kwa kichwa
akiunganisha wavuni kona iliyochongwa na Juma Abdul.
Vikosi vilikuwa:-
Yanga:Deogratius Munis, Nadir Haroub, Juma Abdul, Mwinyi Haji, Kelvin
Yondani/Vicend Andrew, Justine Zulu, Simon Msuva, Thabiti Kamusoko, Donald
Ngoma, Obrey Chilwa na Haruna Niyonzima/Emmanuel Martin.
Stand:Sebastiane Stanley/Mohamed Makaka, Jacob Massawe, Erick Mulilo, Adeyum
Ahmed, Revocatus Richard, Ibrahim Job,
Abdulaziz Makame, Adam Salamba/Kheri Rashid, Frank Khamis, Absalim Chidiebele
na Seleman Selembe.
No comments:
Post a Comment