Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Tuesday, February 7, 2017

HOTUBA YA RAIS TFF, JAMAL EMIL MALINZI KUHUSU SERENGETI BOYS




Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa furaha maamuzi yaliyotolewa na Kamati ya Utendaji ya CAF ya kuipa Tanzania nafasi ya kucheza fainali za Afrika za vijana chini ya umri wa miaka 17 (Afcon U17). Mashindano haya yatanyika nchini Gabon kuanzia tarehe 21 Mei, 2017 hadi 04 Juni, 2017. 
Timu nane zitashiriki fainali hizi na zimegawanywa makundi mawili, kundi A ni Gabon, Ghana, Guinea, Cameroon na kundi B ni Mali, Niger, Angola na Tanzania. Washindi wawili wa kila kundi wataliwakilisha bara la Afrika katika fainali za dunia huko India mwezi Novemba mwaka huu.
Shirikisho la Mpira  wa  Miguu Tanzania linatoa shukrani za pekee kwa Mh. Rais Dr John  Pombe Magufuli kwa jitihada za Serikali kusapoti michezo, tunamshukuru sana Mh. Waziri Mkuu  Kassim Majaliwa Kassim kwa kutupa shime na kufuatilia kwa karibu maendeleo ya timu. Shukrani kwa Mh. Nape Nnauye  na Wizara  kwa  ushirikiano wa karibu aliotupatia wakati wote wa kuandaa timu na kuelekea kwenye mashindano hatua ya mtoano. 
Tunamshukuru sana Bw. Issa Hayatou  Rais wa CAF  na Kamati yake ya Utendaji kwa kututendea haki, Bw. Leodeger Tenga Rais wa heshima wa TFF na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya CAF tunamshukuru na kumpongeza  sana kwa jitihada binafsi alizofanya kuhakikisha haki ya Tanzania haipotei. 
Ninaishukuru sana Kamati ya Utendaji ya TFF, Chama cha Mpira Zanzibar ZFA, Kamati ya Mpira wa Vijana ikiongozwa na Bw. Ayoub Nyenzi, viongozi wa vyama vya mpira vya Mikoa, na Sekretariet ya TFF ikiongozwa na Katibu Mkuu Bw. Mwesigwa Selestine kwa kazi kubwa waliyoifanya kusimamia timu.
 Tunamshukuru Dr. Paul Marealle mjumbe wa Kamati ya Tiba ya CAF na Mwenyekiti wa Kamati ya Tiba ya TFF kwa kufuatilia kwa karibu suala hili na kutoa ushauri wa kitaalam kwa TFF. 
Shukrani za pekee kwa washirika wetu Azam Media, Airtel, Coca Cola na Kampuni ya SS Bakhresa. Mchango wao ni mkubwa katika kufikia mafanikio haya.
Wazazi wa vijana wetu wa Serengeti Boys tunawashukuru kwa kuwaruhusu watoto wao washiriki kwenye mashindano haya. Tunaomba waendelee na moyo huo.
Pongezi nyingi sana kwa wachezaji wetu Serengeti Boys na benchi lao la ufundi kwa kututoa kimasomaso na kuhakikisha bendera ya Tanzania inapeperushwa Gabon mwezi Mei. Kazi kubwa mmeifanya, mmepambana na timu kubwa na mkatoka  mashujaa. Mmeiondoa Seycheles mashindanoni, mkaiondoa timu kubwa ya Afrika Kusini mashindanoni  na mkataoa  sare ya jumla ya mabao 3-3 dhidi ya Kongo na kutolewa  kwa bao la ugenini. Wapinzani wetu Kongo hawakutenda haki kwa kuchezesha wachezaji wakubwa kwa umri. CAF walipowaagiza, si mara moja, ila mara tatu kuwa wamlete mchezaji husika anayetuhumiwa kuzidi umri hawakufanya hivyo na wakatolewa mashindanoni.
 Safari ya kwenda Gabon haikuwa fupi ilikuwa ndefu. Kufuatia maono ya mbali ya TFF safari hii ilianza mwaka 2014 mara tu baada ya mashindano ya Copa Coca Cola ambayo yalihusisha vijana umri chini ya miaka 15 wakati huo. Wachezaji bora katika mashindano hayo walikusanywa pamoja wakawekwa kambini na kuanza mazoezi yaliyoambatana na ziara za mechi za majaribio mikoani. Ni katika ziara hizi vipaji vipya vilionekana na kuongezwa kwenye timu.
TFF inavishukuru sana vyama vya mpira vya India, Seychelles, Madagascar, Rwanda na Korea Kusini kwa kufanikisha kambi za kimataifa za Serengeti Boys. Kambi hizi zilitoa fursa kwa vijana wa Serengeti Boys kupata uzoefu wa kimataifa kupitia michezo ya kujipima nguvu waliyocheza dhidi ya timu kubwa duniani kama Marekani, Korea Kusini, Misri, Malasyia, Madagascar na India.
Tunayashukuru sana makundi yote ya mashabiki wa timu zetu za Taifa kwa kutoa hamasa wakati wote Serengeti Boys ilipocheza. Washiriki mbali mbali kwenye mitandao ya jamii tunawashukuru kwa kufuatilia kwa karibu maendeleo ya timu na kuwatia moyo vijana. Tuendelee na moyo huu.
Vyombo vya habari tunavishukuru sana kwa kutoa taarifa mbali mbali zinazohusu timu, kuandika makala na kuhamasisha vijana.
Sasa tunayo kazi kubwa mbele yetu, kuhakikisha Tanzania inarudi na Kombe toka Gabon. Nimeliagiza benchi la ufundi liandae program ya maandalizi ya timu kuelekea Gabon 2017. Program hii itahusisha kambi ndani ya nchi (ambayo tayari imeanza) na kambi ya angalao mwezi mmoja nje ya nchi, TFF iko mbioni kutafuta kambi hii na karibu tutafanikiwa kuipata, itakuwa ni katika nchi iliyoendelea kisoka.
Serengeti Boys haina mdhamini. Gharama za maandalizi ni kubwa na hazitapungua dola za kimarekani laki nne na zitajumuisha gharama za mechi za majaribio (gharama za mechi hizi hazipungui dola 50,000.- kwa kila mechi), gharama za kambi ndani ya nchi, gharama za kambi nje ya nchi ambazo hazitapungua dola laki moja ($100,000), usafiri wa kwenda na kurudi Gabon,gharama za timu wakati wa mashindano ikiwemo usalama wa timu Gabon,  pamoja na vifaa na matumizi mengine. TFF kupitia mfuko wake wa TFF Football Development Fund itafanya kila jitihada kuhakikisha pesa hizi zinapatikana ili kuhakikisha timu yetu inafanya vizuri Gabon. Hatutaki viwepo visingizio kama ambavyo huwa inatokea kwa nchi nyingine.
Tunatoa wito kwa Serikali, mashirika binafsi na umma, watu binafsi, makundi mbali mbali ya jamii kwa pamoja tushirikiane tuhakikishe kila kinachohitajika kinapatikana ili kuhakikisha mafanikio ya timu. Sekta ya umma na ya binafsi karibu mtoe ushamini kwa Serengeti Boys ili nanyi mkuze jina la biashara zetu. Bahati nzuri jina la Serengeti Boys linachukua jina la moja ya vivutio vyetu vikubwa vya utalii, hii ni fursa kubwa ya kutangaza jina la nchi yetu na vivutio vyake vya utalii kupitia timu hii na fainali hizi za Afrika.
Fainali hizi za Afrika zitakuwa ni fursa pekee kwa wachezaji wa Tanzania kuingia kwenye anga za Kimataifa. Wachezaji wengine wakubwa duniani wakiwemo kina John Obi Mikel, Celestine Babayaro, Nwanko Kanu, Kelechi Ihenacho, Samuel Kuffour, Nii Lamptey, Michael Essien wametokea kwenye fainali hizi.
Ushiriki wa Tanzania katika fainali hizi itakuwa ni fursa ya pekee ya kuwa hamasisha wadau wa mpira wa miguu Tanzania ili na sisi tuweze kuanda  fainali zijazo nzuri za Afrika za vijana chini ya umri wa miaka 17 mwaka 2019. Tanzania ni mwenyeji wa fainali hizi. Siku ya fainali ya Gabon  Afcon U17 kabla ya kombe kutolewa  Tanzania tutakabidhiwa rasmi utambulisho  wa kupokea mashindano haya toka kwa Gabon .
Ninaomba nimalizie kuwaomba Watanzania wenzangu timu yetu ya Serengeti Boys tuiweke kwenye sala na dua zetu ili izidi kupata mafanikio.
Mungu ibariki Serengeti Boys.
Mungu ibariki Tanzania.
Mungu ibariki Afrika.
Ahsanteni sana.
Jamal Malinzi
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).


No comments:

Post a Comment