SIMBA, imerejea kileleni mwa Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara baada ya kuifunga Ndanda
FC ya Mtwara kwa mabao 3-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Imerejea
kileleni baada ya Jumanne wiki hii kuenguliwa na bingwa mtetezi Yanga
aliyeipiga African Sports kwa mabao 5-0 na kufikisha pointi 50, ilihali Simba
ikifuatia kwa kuwa na pointi 48. Lakini ushindi wa jana umeipaisha tena Simba
na kufikisha pointi 51 na mabao 40. Yanga ina mabao 51 wakati timu inayoshika
nafasi ya tatu ni Azam FC yenye pointi 47, lakini ikiwa imecheza mechi mbili
pungufu. Simba imecheza mechi 22 wakati Yanga imecheza mechi 21. Katika mchezo
wa jana, Simba ilipata bao la kwanza katika dakika ya 36, mfungaji akiwa Mwinyi
Kazimoto aliyeunganisha kwa shuti kali wavuni krosi ya Hassani Kessy. Bao hilo
lilidumu hadi mapumziko. Mabao mengine ya Simba yalipatikana katika kipindi cha
pili, mfungaji akiwa raia wa Uganda aliyeichezea Yanga hadi msimu uliopita,
Hamisi Kiiza. Alifunga bao la pili katika dakika ya 57 kwa kichwa, baada ya
kuifuata kiufundi mpira wa kona uliopigwa na Ibrahim Ajibu ambaye dakika 11
baadaye alipumzishwa na nafasi yake kuchukuliwa na Danny Lyanga. Bao la tatu
kwa Simba lilifungwa katika dakika ya 72, baada ya Kiiza kuinasa pasi ya Lyanga
na kuupachika mpira kimiani. Kabla ya mpira kumfikia Lyanga na kutoa pasi,
kiungo Justice Majabvi aliachia shuti kali lililotemwa na kipa wa Ndanda mna
mpira kumfikia Lyanga. Hata hivyo, ushindi huo haukuwa mwepesi kwa Simba, kwani
Ndanda iliyokuwa na nyota kama Atupele Green, Kigi Makasi, Omega Seme,
Salvatory Ntebe na wengine, licha ya kufungwa walionesha kandanda safi. Matokeo
hayo yanaiacha Ndanda katika nafasi yake ya nane, ikiwa na pointi 24 ilizovuna
katika michezo 21. Kikosi cha Simba: Vicent Angban, Hassan ramadhani, Mohamed Hussein,
Novaty Lufungo, Juuko Murshid, Justine Majabvi, Mwinyi Kazimoto, Jonaes Mkude,
Hamisi Kiiza, Ibrahim Ajib na Said Ndemla. Ndanda Kuchele: Jeremias Kisubi,
Azizi Sibo, Paulo Ngalema, Kassian Ponela, Salvatory Ntebe, Hemed Khoja,
William Lucian, Omega seme, Omary Mponda, Atupele Green na Kigi Makasi.
No comments:
Post a Comment